TARI YASHIRIKI MKUTANO WA WADAU WA KOROSHO DUNIANI.
TARI YASHIRIKI MKUTANO WA WADAU WA KOROSHO DUNIANI
Mkurugenzi Mkuu wa TARI Dkt. Thomas Bwana pamoja na Timu ya watafiti kutoka TARI Naliendele wako nchini Dubai kuhudhuria mkutano wa Dunia wa Wadau wa Korosho (World Cashew Conference) ikiwa ni fursa ya kushiriki majadiliano, kujifunza na kufahamu muelekeo wa zao la korosho Duniani.
Mkutano huo wa siku tatu (tarehe 30 Januari – 1 Februari) pamoja na mambo mengine umejadili mambo mbalimbali kuhusu muelekeo wa zao la korosho, changamoto pamoja na fursa zilizopo katika maendeleo ya teknolojia mbalimbali katika tasnia ya zao la korosho.
Mkutano huo ambao umekutanisha wadau kutoka nchi mbalimbali Duniani katika mnyororo wa thamani utasaidia TARI kuwa na mwelekeo sahihi wa kazi za utafiti wa zao la korosho ili kukidhi malengo ya soko la Dunia.
Vilevile katika Mkutano huu TARI imefanikiwa kufanya majadiliano na baadhi ya Taasisi na washirika wa maendelea kama GIZ, ACA na CHINA chamber of Commerce na kupenyeza mapendekezo na mawazo ya kitafiti ili kupata uwezeshaji katika maeneo mbalimbali ya kitafiti
Washirika wa Maendeleo GIZ watafadhili miradi 2 kwenye zao la korosho. Aidha, TARI inaangalia uwezekano zaidi wa kupata ufadhili wa GIZ kwenye masuala ya CARBON CREDIT kwenye korosho na mazao mengine
Katika hatua nyingine, TARI imepanga kushirikiana na Taasisi ya African Cashew Alliance katika kuandaa program ya mafunzo ili kuwajengea uwezo watafiti katika tasnia ya korosho.
Timu ya TARI iliyoambatana na Mkurugenzi Mkuu wa TARI katika Mkutano huo ni pamoja na Mkurugenzi wa Kituo cha TARI Naliendele Dkt. Geradina Mzena, Mtafiti kiongozi wa zao la korosho Dkt. Wilson Nene na Mratibu wa Uhaulishaji Teknolojia Bw. Bakari Kidunda.
TARI kupitia Kituo chake cha TARI Naliendele wana jukumu mahsusi Kitaifa la kufanya utafiti wa zao la korosho katika mnyororo wa thamani.